Thursday, October 10, 2013

TAARIFA YA WAZIRI WA NCHI OFISI YA MAKAMU WA PILI WA RAIS MHESHIMIWA MOHAMED ABOUD MOHAMED KUHUSU UJENZI WA MNARA WA KUMBUKUMBU YA MIAKA 50 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR


Ndugu Wananchi;

Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujaalia amani, umoja, mshikamano na utulivu, jambo ambalo linazidi kutusaidia katika kupiga hatua za maendeleo ya kijamii na uchumi katika nchi yetu.

 Kama sote tunavyoelewa, nchi yetu hivi sasa imo katika shamra shamra za Maadhimisho ya miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Mapinduzi ya Januari 1964 ni mapinduzi yaliyoikomboa nchi yetu kutoka katika mikono ya kikoloni na kujenga usawa wa wananchi wote bila ya kujali tofauti zao za kikabila, rangi, imani za dini na mahala wanakotoka. Aidha, Mapinduzi yameweza nchi yetu kupiga hatua za haraka katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni. Sote kwa pamoja tunashuhudia na kufaidika na matunda ya Mapinduzi, hivyo katika kuadhimisha kutimia miaka 50 ya Mapinduzi, wananchi wote tunawajibu wa kushiriki kikamilifu katika maandalizi na kuadhimisha siku hii adhim kwetu.
 Katika maadhimisho ya Sherehe zetu hizi, Serikali imepanga kutekeleza shughuli mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa Mnara Maalum wa Kumbukumbu ya Kutimiza Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar. Mnara huu utajengwa katika eneo la Michenzani, mbele ya nyumba nambari 2 pembeni mwa Maskani ya Kisonge
Mnara wa Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Mapinduzi utakuwa ni kielelezo (landmark) cha nchi yetu na unakusudiwa kuwa ni moja ya vivutio vya utalii na sehemu ya kusoma historia ya Mapinduzi. Serikali ina azma ya kuliendeleza eneo la Michezani kuwa eneo la kisasa kwa kuweka bustani ya kisasa, kuimarisha miundombinu ya barabara, maegesho ya magari na maduka ya biashara.

Ujenzi wa minara kama hii si jambo geni duniani, tumeshuhudia kujengwa kwa minara maarufu kama mnara ulioko Paris, Ufaranza; Shangai, China na mingine mingi ambayo Miji na Nchi iliyopo minara hiyo hujipatia umaarufu na hivyo kuvutia watu wa mataifa mbalimbali kwenda makusudi kuitembelea.
Eneo la Michenzani limechaguliwa kutokana na historia ya eneo hilo ambalo linaushahidi wa wazi wa matunda ya mapinduzi. Miongoni mwa matunda hayo ni kuwepo kwa nyumba za maendeleo na bara bara za kisasa zilizojengwa mara tu baada ya Mapinduzi.


Ujenzi wa Mnara katika eneo hili la Michezani utafungua njia kwa shughuli nyengine za kimaendeleo na hivyo kuleta haiba nzuri ya eneo hilo na Mji wa Zanzibar kwa ujumla. Aidha, kuimarika kwa eneo la Michenzani kutatoa fursa kwa Wananchi walio wengi kujiajiri kutokana na kufanya biashara katika eneo hilo na kupungunza mrundikano wa watu katika eneo la Darajani.

Tunaelewa kuwa eneo litakalojengwa mnara huo tayari wananchi wenzetu walikuwa wanalitumia kwa shughuli mbalimbali. Tunawaomba wananchi wote kuelewa kuwa eneo hilo sasa limo katika harakati za ujenzi na tunawaomba kutoa ushirikiano kwa kuondoka katika maeneo hayo ili kupisha shughuli ya kimaendeleo na kihistoria katika nchi yetu.
Kabla ya kumalizia naomba nichukue fursa hii kuwaomba wananchi wote kushiriki katika shughuli mbali mbali za maadhimisho katika maeneo yetu. Na pia nawaomba Taasisi za Serikali na Sekta Binafsi, na Wajasiriamali kujitayarisha vyema kushiriki katika Maonyesho ya aina yake yatakayofanyika katika Viwanja vy Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA) Kampasi ya Beit El Raas.  Katika Maonyesho haya Taasisi mbali mbali zitaonyesha mafanikio ya Taasisi zao katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.

 

“Tudumishe Amani, Umoja na Maendeleo ambayo ni Matunda ya Mapinduzi yetu – Mapinduzi Daima”

Ahsanteni
Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Pili  wa Rais, Zanzibar

No comments:

Post a Comment